Header

“Inapaswa kumgeukia Mungu kwa kutubu dhambi na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo” (Matendo 20:21).

 

“Je, ninahitaji kufanya nini ili niokoke?”  Pengine wewe umejiuliza swali hili mara mingi.  Unajua kwamba hujaokoka.  Unajua kwamba bado uko ndani ya dhambi zako na unajua kwamba ukifa katika hali hii basi bila shaka utatupwa jahanum.  Unajua kwamba Mungu ni mtakatifu na mwenye haki na ukiendelea kukaa katika hali hii, Yeye hatakuruhusu kuingia mbinguni.  Je, ni nini unahitaji kufanya ili uokoke?

 

Katika mstari huu tunaambiwa ni nini mtume Paulo alihubiri wakati aliwatembelea watu katika manyumba zao.  Aliwaambia, “Inapaswa kumgeukia Mungu kwa kutubu dhambi na kumwamini Bwana wetu Yesu Kristo.”

 

1.  Inapaswa kumgeukia Mungu kwa kutubu.

 

Jambo la kwanza kila mtu anahitaji kufanya akitaka kuokoka ni kutubu dhambi zake.  Je, kutubu kunamaanisha nini?  Kutubu kunamaanisha mambo mawili.

Kwanza, kutubu kunamaanisha kukubali kwamba wewe ni mwenye dhambi na kwamba wewe mwenyewe huna uwezo wa kujiokoa.  Unahitaji kufahamu kwamba wewe huna chochote kizuri ndani yako na wewe huna uwezo hata kidogo wa kumpendeza Mungu kwa matendo yako.  Hata kama unajaribu sana kumpendeza Mungu kwa matendo yako, hutafaulu.  Unahitaji kufahamu kwamba wewe ni mtenda dhambi.  Hili ni jambo ambalo wewe unahitaji kukubali wakati unakuja mbele za Mungu kwa maombi.  Usijaribu kumwambia kwamba wewe ni mtu mwema, bali kubali mbele zake kwamba wewe  uko na moyo wa dhambi na wewe uko na hatia ya dhambi mbele zake.

 

Pili, kutubu kunamaanisha kugeuka kutoka kwa dhambi na kuendelea kugeuka.  Haitoshi kukubali tu kwamba wewe ni mwenye dhambi.  Kukubali peke yake haitakuokoa.  Unahitaji kuamua kwamba utageuka kutoka kwa dhambi zako.  Unahitaji kuamua kwamba utaacha milele dhambi zako zote.  Unahitaji kufanya hii maisha yako yote.  Mungu anaamuru kwamba kila mmoja ambaye anakuja kwake kuomba wokovu ataamua kuacha dhambi zake.  Mungu ni Mtakatifu na mwenye haki na msafi kabisa.  Yeye hatapokea wale ambao wanapenda dhambi zao na hawataki kuziacha.  Yeye atawapokea wale tu ambao wameamua kutoroka dhambi zao.

 

2.  Unahitaji kumwamini Yesu Kristo pekee akuokoe kutoka kwa dhambi zako.

 

Ukitaka kuokoka, unahitaji kugeuka kutoka kwa dhambi zako, na kumgeukia Kristo.  Unahitaji kuja kwake Kristo kwa imani na kumtumainia Yeye pekee kwa wokovu wako.  Unahitaji kwenda kwake kwa maombi na kukubali kwamba wewe huwezi kujiokoa.  Unahitaji kumwomba akuokoe.  Unahitaji kumwomba aondoe deni la dhambi zako na kukuosha katika damu Yake.  Unahitaji kumwomba akuondoe kutoka kwa nguvu za dhambi na aondoe ghadhabu ya Mungu ambayo iko juu yako.

 

Biblia inatuambia, “Kristo Yesu alikuja ulimwenguni kuokoa wenye dhambi” (1 Timotheo 1:15).  Hili ndilo lilikuwa lengo lake la kuja hapa ulimwenguni.  Aliishi maisha kamili ili sisi tuweze kuwa wenye haki kupitia kwa imani ndani yake.  Yeye alikufa juu ya msalaba kulipa deni la dhambi zetu.  Alimwaga damu Yake ili sisi tuweze kuoshwa na kukombolewa kutoka kwa utumwa wa dhambi.  Alikufa juu ya msalaba kuondoa ghadhabu ya Mungu ambayo ilikuwa juu yetu.  Yeye aliteswa ili sisi tuweze kusamehewa, Yeye alikufa ili sisi tuweze kuwa na uzima.  Yeye pekee ndiye njia ya kupata msamaha na kuoshwa na kuokoka.  Yeye pekee alitumwa na Mungu hapa ulimwenguni kuwaokoa wenye dhambi.  Yeye pekee alikufa kwa ajili ya wenye dhambi.

3.  Ni lazima utubu na kumwamini Kristo leo.

 

Umeona kwamba ukitaka kuokoka unahitaji kugeuka kutoka kwa dhambi zako na kumgeukia Kristo.  Ni lazima ufahamu kwamba unahitaji kufanya hii leo.  Usisema, “Siku moja kweli nitaokoka.”

 

Unahitaji kuja kwake Kristo leo kuokoka kwa sababu hujui kama utapata nafasi ya kuja kwake Kristo siku nyingine.  Kumbuka kwamba kila siku moyo wako unaendelea kuwa mgumu kwa sababu ya dhambi zako.  Kila siku moyo wako unapenda dhambi zaidi na zaidi.  Ukiacha jambo hili la kuokoka pengine siku moja hutaweza kutubu na kuamini kwa sababu moyo wako umekuwa mgumu sana.

 

Kumbuka pia kwamba wewe hujui ni siku gani utakufa.  Pengine leo wewe ni kijana na uko na afya.  Lakini hii haimaanishi utaishi hapa miaka mingi.  Wengi wanakufa wakiwa vijana.  Jambo hili ni la muhimu sana, usiliache.  Njoo kwake Kristo leo na utaokoka.